Rais Jakaya Kikwete akisalimia na Waziri wa Uchukuzi, Dkt Harrison Mwakyembe wakati akiingia katika uwanja wa Julius Nyerere International Airport (JNIA) kuweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa jengo la tatu la abiria jijini Dar es Salaam.


.Asema kama Rais wa nchi inamuuma sana kwa taifa kuwa uchochoro wa dawa hizo
.Rais asema watumishi wanaojihusisha na dawa za kulevya kuondolewa mara moja
.TAA watengeneza jengo jipya la abiria lenye mifumo ya kimataifa


RAIS Jakaya Kikwete ametoa maagizo ya haraka ya utayarishaji mpya wa mfumo (Procurement) wa ulinzi katika viwanja vyote vya ndege nchini katika harakati za kudhibiti usafirishaji na uigizaji wa madawa ya kulevya Tanzania. Moblog inaripoti.

Rais Kikwete alitoa rai hiyo katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa jengo la tatu la abiria Julius Nyerere International Airport (JNIA) jijini Dar es Salaam kwa kusema inakera sana kuona wasafirishaji wa dawa za kulevya kukamatwa Afrika ya Kusini.

“sisi wengine tunaumia sana kusikia msanii fulani au mwanamuziki kukamatwa na dawa za kulevya nchini Afrika Kusini, mtu unajiuliza kapitaje hapa uwanja wa ndege dar au kwa kuwa msanii tu lakini inakera na ninaumia sana,’ amesema Rais Kikwete.





Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza jana, Alhamisi, Aprili 24, 2014, kabla ya kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Awamu ya Tatu ya Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere wa Dar es Salaam kwenye eneo la Uwanja huo, Kipawa.


Amesema lazima mamlaka za viwanja vya ndege kwa kushirikiana na wizara na wadau wengine waunganishe nguvu zao katika kupambana tatizo hili la dawa za kulevya kwa kuwa linaichafua nchi nzima kimataifa na kikanda.

Rais Kikwete aliongeza kwamba lazima mamlaka zinazohusika zianze mara moja kutengeneza mfumo madhubuti wa ulinzi katika viwanja vya ndege hasa wa Dar es Salaam na KIA kule kilimanjaro ambazo ndio njia kuu za usafirishaji wa madawa hayo.

Amesema lazima kasi ya kupambana na usafirishaji na uigizaji wa dawa za kulevya kupitia viwanja vya ndege iongeze na siyo kusuasua miaka miwili au mitatu ya kutengeneza mifumo ya ulinzi ya kimataifa.


Rais Kikwete amesema kwamba kama kuna watumishi wa idara ya forodha (TRA), Mambo ya Ndani au Polisi wanaoshirikiana na wauza madawa ya kulevya apewe majina yao na watashughulikiwa mara moja.


“tusimuonee haya mtu yeyote hata kama ni mtumishi wa umma kwa sababu tunaonekana wote tunajishughulisha na biashara hiyo haramu ni lazima tuchukue hatua madhubuti,” aliongeza Rais





Rais Kikwete akisisitiza jambo baada ya kuona uchoro wa jengo jipya la abiria na mfumo wa ulinzi kutoka, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, Injia Suleiman Suleiman (mwenye tai nyekundu).

Kwa upande wake, Waziri wa Uchukuzi, Dkt Harrison Mwakyembe akizungumza na mwandishi wa habari hizi muda mfupi baada ya Rais kuweka jiwe la msingi amesema kuwa tayari Mamlaka ya viwanja vya ndege (TAA) wameshaweka mifumo hiyo yaani (Procurement) katika kudhibiti dawa za kulevya.

Amesema kuwa katika jengo jipya la abiria (Terminal three) kuna hatua tano za kukagua madawa ya kulevya na aina nyingine ya vitu visivyoruhusiwa katika uwanja wa ndege kwa hiyo serikali imejipanga kumaliza kabisa tatizo hili nchini.


“kimsingi mifumo hii ipo tayari katika jengo hili jipya la abiria na kama kuna mtu atapitisha dawa za kulevya basi nitampa zawadi ya fedha,’ amesema Dkt Mwakyembe


Dkt Mwakyembe alisisitiza kwamba katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya lazima wizara na TAA watashirikiana na wadau wengine kama vile Mamlaka ya Mapato (TRA) kupitia idara ya forodha, wizara ya mambo ya ndani yaani Polisi na Idara ya Usalama wa Taifa (TISS).


Hayo yanakuja wakati taarifa zilizopo ni kwamba wasafirishaji wa dawa za kulevya kuanza kutumia fukwe ndogondogo za bahari nchini kuziingiza kutoka Mashariki ya mbali.




Rais Jakaya Kikwete akikata utepe ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa kuanza ujenzi wa jengo la tatu la la Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam. Kutoka kushoto ni Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk. Charles Tizeba , Balozi wa Uholanzi nchini, Jaap Frederiks, Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Injinia Suleiman Suleiman, na Mwenyekiti wa Kamatim ya Bunge ya Uchukuzi Mhe. Peter Serukamba.



Rais Kikwete pamoja na Balozi wa Uholanzi nchini Mhe Jaap Frederiks baada ya kuweka jiwe la msingi na kuashiria ujenzi wa jengo jipya umeanza rasmi.

chanzo:Mo blog Tanzania